Hakikisheni vikundi vinavyopatikana kwaajili ya kupewa mikopo, visiwe vikundi chechefu kwa kuwa havina tija na baadae vinatuletea usumbufu katika kurejesha Fedha; hivyo simamieni vikundi hivyo ili kupata vikundi vyenye tija kwa kuhakikisha vinapitia kila hatua stahiki Kabla ya kupewa mikopo hiyo.
Hayo yamesemwa leo Desemba 5, 2025 na Ndg. Muhksin Kassim Katibu Tawala wa Wilaya ya Monduli, wakati akizungumza na Maafisa Maendeleo ya Jamii Wilayani humo ambao ndio kundi muhimu katika suala la usimamizi na ufuatiliaji wa vikundi vinavyostahili kupewa mikopo kwa makundi ya Wanawake, Vijana na watu wenye ulemavu hasa kwa kipindi hiki cha siku 100 tangu Mhe. Rais ameingia madarakani ili panapofika Tathmini ya suala la utoaji mikopo; Halmashauri hiyo iweze kufanya vizuri kwa kuwa karibu na wananchi, kusikiliza na kutatua changamoto zao.\n\nAidha Ndg.Muhksin Kassim amewataka maafisa Maendeleo ya Jamii hao, kuhakikisha vikundi hivyo havisambaratiki lakini pia wavifahamu; si tu kujua idadi ya vikundi hivyo, bali pia kufahamu Vilipo na shughuli zinazofanyika kwa kila kikundi kwani kwa kufanya vizuri wao, hata Serikali inapata sifa na kinyume chake Serikali inalaumiwa.
Naye Bi.Happiness R. Laizer Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya hiyo, amewataka Maafisa Maendeleo ya Jamii kuwahi kazini, kufuata taratibu, Sheria na Kanuni za serikali na kwamba kundi la Maafisa hao ni muhimu sana katika mchakato wa utoaji wa mkopo kwa vikundi vya wanawake, Vijana na watu wenye ulemavu.
Sambamba na hayo ameishukuru serikali kwa kuipatia halmashauri hiyo maafisa maendeleo ya jamii( ajira mpya) na kuongeza idadi yao katika kata na kuwataka kutoa ushirikiano kwa Timu ya utoaji mikopo wakati wa ukaguzi ili kusiwe na malalamiko.\n\nKwa upande wake Bi.Lidya Mauki ambaye ni Mkuu wa TAKUKURU Wilaya ya Monduli amewaeleza Maafisa Maendeleo ya Jamii kuwa uadilifu ni nguzo muhimu katika kuzuia vitendo vya rushwa hivyo wanao wajibu wa kuwaelimisha wananchi juu ya vitendo vya rushwa na kuepuka kuwa sababu ya kuwafanya wananchi kuichukia Serikali.
Monduli District Council
Sanduku la Posta: P.O BOX 1 Monduli
Namba ya simu: +255 - 27- 2538006
simu ya mkononi:
Barua Pepe: ded@mondulidc.go.tz
Hatimiliki @2017 Halmashauri ya Wilaya ya Monduli